MATOKEO YA SENSA KATIKA MIFUMO MITATU YA IKOLOJIA

Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe.Angellah Kairuki ametangaza rasmi matokeo ya sensa ya wanyamapori katika mifumo mitatu ya ikolojia ya Nyerere-Selous-Mikumi, Saadani-Wamimbiki na Serengeti ambayo ni miongoni mwa mifumo 11 ya ikolojia nchini.

Akitangaza matokeo hayo katika mkutano wa wadau wa uhifadhi na utalii uliofanyika jijini Arusha, Mhe. Kairuki amesema, sensa katika mfumo ikolojia wa Nyerere-Selous-Mikumi, unaonesha kuimarika kwa spishi 22 za wanyamapori wakiwemo nyati/buffaloes (59,878), tembo/elephants (20,006), nyumbu/wildebeest (19,060), kongoni/hartebeest (18,361), swalapala/impala (14,031), ngiri (13,806) na idadi ya Wanyama walioonekana kwa idadi ndogo ni twiga/giraffe (1,679), Tandala mkubwa/greater kudu (1,414) na puku/sheshe (496).

” katika mfumo huu kumekuwa na ongezeko la tembo 20,006 (2022) ikilinganishwa na sensa ya awali 15,501 (2018) na Viashiria vya ujangili wa tembo au vifo vya tembo vimepungua kwa kiasi kikubwa kutoka 16% mwaka 2018 hadi hadi 0.8% mwaka 2022″ ameeleza Mhe.Kairuki

Mhe.Kairuki ameitaka Idara ya Wanyamapori Wizara ya Maliasili na Utalii kuchukua hatua za haraka kulinda idadi ya Sheshe/puku ambao wanapatikana Tanzania pekee waliosalia katika maeneo yao ya asili yakiwemo mapori ya akiba ya Kilombero na ziwa Rukwa ambao idadi yao imepungua kwa kiasi kikubwa kutoka (1,579 mwaka 2018) hadi (496 mwaka 2022).

Vilevile , uhesabuji wa Nyumbu katika mfumo ikolojia wa Serengeti
Matokeo ya sensa hii yamebaini uwepo wa nyumbu wanapatao 1,597,850. Idadi hii inaonyesha kuimarika kwa nyumbu ikilinganishwa na sensa ya hapo awali (2015) iliyoonyesha uwepo wa nyumbu wapatao 1,326,709.

Kwa upande wa mfumo ikolojia wa Saadani – Wami – Mbiki Matokeo ya sensa yameonesha uwepo wa wanyamapori wachache unahusishwa na hali ya upya wa hifadhi hizi ambapo hapo awali,hifadhi ya Saadani ilikuwa pori tengefu na sehemu nyingine ilikuwa shamba la mifugo na zoezi la kuongeza wanyamapori lilifanyika miaka ya hivi karibuni .

Aidha ,Mhe. Kairuki amesema kwa mwaka wa fedha 2024-2025 wizara imeweka mikakati ya kufanya sensa ya wanyamapori katika mifumo yote ya ikolojia kwa lengo la kuimarisha uhifadhi na kukuza kuwa na utalii endelevu ambapo ametoa rai kwa wadau kuonga mkono jitihada hizi za Serekali katika kuhifadhi utajiri wa Maliasili ya Wanyamapori .

Visitors

015691
Users Today : 4
Users Last 7 days : 570
Users This Month : 268
Total Users : 15691

Office Location

Contact Us